Jumamosi, 26 Oktoba 2013

KUJA KWA YESU KRISTO MARA YA PILI DUNIANI NA VITA YA HAR-MAGEDONI

Neno la Uzima kutoka kwa Askofu Zachary Kakobe

Tovuti : www.bishopzacharykakobe.org

Facebook : www.facebook.com/bishopkakobeministries

Youtube : www.youtube.com/user/bishopkakobe

SOMO: KUJA KWA YESU KRISTO MARA YA PILI DUNIANI NA VITA VYA HAR-MAGEDONI

Tuliangalia katika masomo yaliyopita kwamba, Dhiki kubwa au Dhiki kuu, itachukua kipindi cha miaka saba ( 7 ). Katika kipindi hiki pia, watakatifu walionyakuliwa wakati wa kunyakuliwa kwa kanisa, watakuwa katika kipindi cha kupewa taji na kufanyiwa karamu ya harusi ya MwanaKondoo. Ni makusudi ya somo letu la leo kujifunza tukio litakalofuata mwisho wa miaka hii saba, Kuja kwa Yesu Kristo mara ya pili duniani na Vita vya Har-Magedoni. Tutaligawa somo letu la leo katika vipengele vitano:-

( 1 ). KUJA KWA YESU KRISTO MARA YA PILI DUNIANI.

( 2 ). TOFAUTI YA KUJA KWA YESU WAKATI WA KUNYAKULIWA KWA KANISA NA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI

( 3 ). MAKUSUDI YA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI

( 4 ). TAIFA LA ISRAELI WAKATI WA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI.

( 5 ). VITA VYA HAR-MAGEDONI NA KUFUNGWA KWA SHETANI MIAKA ELFU MOJA.

( 1 ). KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI.

Yesu Kristo, mara ya kwanza, alikuja hapa duniani katika udhaifu na unyonge kwa kuzaliwa na Mariamu na kulazwa katika Hori kulia ng’ombe. Kwa Waisraeli ambao hawakujua maandiko vema, hawakutambua kwamba Kristo Kristo ni Yesu kutokana na mazingira yake ya umaskini na unyonge ( LUKA 9:58; 2 WAKORINTHO 8:9 ). Walidhani wakati ule wa kwanza angekuja kama Mfalme na kushindwa kafahamu kwamba wakati wa kuja kama Mfalme, ilikuwa wakati wa kuja kwake MARA YA PILI duniani. Wakati wa kuja kwa Yesu mara ya pili, atakuja katika mazingira tofauti kabisa na pale mwanzoni. Atakuja na hali zifuatazo:-
1. Atakuja kama UMEME ( MATHAYO 24:27 ).
Atakuja pamoja na malaika wa uweza ( 2 WATHESALONIKE 1:7 ).
Atakuja katika MWALI WA MOTO ( 2 WATHESALONIKE 1:7-8 ).
Atakuja juu ya mawingu pamoja na nguvu na utukufu mwingi (MATHAYO 24:30; 25:31 ).
5. Atakuja kama MFALME WA WAFALME, NA BWANA WA MABWANA ( UFUNUO 19:16 )

HALI HALISI YA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI.

Mara tu baada ya Harusi ya MwanaKondoo, mwishoni mwa ile miaka saba, Yesu Kristo atawachukua watakatifu wote aliowanyakua na kuanza nao safari kuja duniani. Atakuwa amepanda Farasi mweupe akituongoza. Sisi nasi, kila mmoja atakuwa amepanda Farasi mweupe tukimfuata maelfu kwa maelefu pamoja na malaika ( YUDA 1:14; UFUNUO 19:11-14 ). Atakuwa amezungukwa na mwali wa moto na atakuja kama umeme unaoonekana pande zote. Mara tu tutakapoanza safari,jua litatiwa giza na mwezi hautatoa mwanga, na nyota zitaanguka kutoka mbinguni kwa kupamba sherehe ya Kifalme. Nyota hizi ni zile zipitazo upesi mawinguni ( METEORS ) au kwa Kiswahili “VIMWONDO” ( MATHAYO 24:29-30 ). Atakuja na kukanyaga mlima Mizeituni, mahali palepale alipopaa kwenda mbinguni wakati alipotoka duniani mara ya kwanza ( MATENDO 1:10-12; ZEKARIA 14:4-5 ). Kazi ya kwanza atakayofanya, itakuwa kuwatuma malaika kuwakusanya Waisraeli wote waliotawanyika duniani kote wakikimbia dhiki nzito juu ya Israeli katika ile miaka mitatu na nusu ya mwisho ( 3.5 ) ya Dhiki Kubwa. Wale wote waliokwepa kupotezwa na Kristowa uongo. Mpinga Kristo, watakusanywa ( MATHAYO 24:23-27, 29-31 ).

( 2 ). TOFAUTI YA KUJA KWA YESU WAKATI WA KUNYAKULIWA KWA KANISA NA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI.

Kabla hatujaendelea na somo letu, ni muhimu kufahamu tofauti ya kuja kwa Yesu wakati wa kunyakuliwa kwa kanisa na kuja kwa Yesu mara ya pili duniani. Haya ni matukio mawili tofauti:-
KUJA KWA YESU WAKATI WA KUNYAKULIWA KANISA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI
1. Anakuja kama Bwana Arusi kumchukua Bibi Arusi wake kanisa tukufu lisilo na waa wala doa ( WAEFESO 5:27; YOHANA 14:1-3 ) 1. Bwana Arusi Yesu Kristo, anakuja PAMOJA na Bibi Arusi kutoka huko juu na kuja hapa duniani kutawala pamoja na Watakatifu wake ( YUDA 1:14; UFUNUO 1:7 )
2. Anakuja na kukutana na Watakatifu wakemawinguni, hatakanyaga dunia. Walioko duniani HAWATAMWONA wakati huu (1 WATHESALONIKE 4:17). 2. Anakuja duniani na kukanyaga Mlima Mzeituni. Walioko duniani WATAMWONA ( ZEKARIA 14:4-5; MATHAYO 24:27 ).
3. Kunyakuliwa kwa kanisa ni kabla ya Dhiki Kubwa ( UFUNUO 3:10; LUKA 21:22-23, 34-36; 1 WATHESALONIKE 1:10 ) 3. Kuja kwa Yesu Kristo mara ya pili duniani ni mara BAADA ya Dhiki Kubwa ( MATHAYO 24:29-30; 2 WATHESALONIKE 2:1-4 )


( 3 ). MAKUSUDI YA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI
Kuwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu

( 2 WATHESALONIKE 1:8; YUDA 1:14-15 ).
Kuwakusanya Waisraeli na kuwabagua Waisraeli ( kondoo ) mbali na mataifa waliosalia

Katika dhiki kubwa ( mbuzi ). Waisraeli wote watakaokusanywa , wataokolewa na Yesu

( MATHAYO 24:31; ISAYA 11:12; MATHAYO 25:31-34; WARUMI 11:25-31 )
3. Kutawala mataifa yote duniani miaka 1,000, pamoja na watakatifu wake kama Mfalme wa Wafalme na Bwana wa Mabwana ( UFUNUO 11:15; UFUNUO 2:26; 5:10; 20:4-5 ).

( 4 ). TAIFA LA ISRAELI WAKATI WA KUJA KWA YESU MARA YA PILI DUNIANI

Wana wa Israeli au Wayahudi, watabadilisha kabisa msimamo wao kuhusu Masihi Yesu

Kristo . Watalia kwa uchungu na kuomboleza huku wakijilaumu kwa nini walimkataa na

Kumchoma kwa mkuki ubavuni, na kisha watamkubali kuwa masihi na mwokozi wao

( UFUNUO 1:7; ZEKARIA 12:10-14; ZEKARIA 13:6; ISAYA 13:9 ). Ndipo hapo Israeli

Kama Kondoo, watabaguliwa na kuingia katika Ufalme wa Mungu.

( 5 ). VITA VYA HAR-MAGEDONI NA KUFUNGWA KWA SHETANI MIAKA ELFU MOJA. Kabla ya Utawala wa Kristo miaka elfu moja ( 1,000 ) duniani pamoja na watakatifu wake, kutatokea vita ijulikanayo kama VITA YA HAR-MAGEDONI ( UFUNUO 16:14,16 ). Vita hivi vitatokana na mpango wa Shetani wa kutaka kuchukua Ufalme kutoka kwa Yesu Kristo kama alivyojaribu kufanya mbinguni (UFUNUO 12:7-8 ). Kabla ya kuja kwa Yesu mara ya pili duniani, kwa jitihada za pamoja, Shetani, Mpinga Kristo (mnyama), na Nabii wa uongo; watatumia roho chafu ambazo zitawaandikisha watu mataifa waliobaki katika dhiki kubwa kutoka duniani kote na kuwaweka tayari kwa vita ili wapigane na majeshi ya Yesu Kristo mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har-magedoni. Hapa ni bonde la Megido ambalo limekuwa mahali pa vita muda mrefu. Bonde hili lipo kusini magharibi mwa mlima wa KARMELI ( 2 NYAKATI 35:22; ZEKARIA 12:11; 1 WAFALME 18:17-19 ). Katika vita hiyo, kutakuwa na mauaji makuu. Wenye dhambi watauawa kwa maangamizo makuu ( UFUNUO 17:12-14; 14:19-20; 19:11-21; ISAYA 13:9; 29:5-8 ). Hapo tutamwona Yesu akiwa mtu wa Vita na Bwana wa Vita halisi ( KUTOKA 15:3 ). Baada ya vita hivi, Shetani atashikwa na kufungwa miaka elfu moja ( UFUNUO 20:1-3 ), na hapo ndipo utakapoanza Utawala wa miaka elfu moja (1,000 )wa Yeesu Kristo duniani.

……………………………………………………………………………………………

Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni? Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14). Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27). Kinyonge ni kipi? Ni yule anayetenda dhambi. Huyu ni mtu asiyefaa, ni mnyonge! Je, wewe ni mtakatifu? Jibu ni la! Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13; YOHANA 14:6). Je, uko tayari kutubu sasa ili upate rehema hii? Najua uko tayari. Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni; “Mungu Baba asante kwa ujumbe huu. Hakika mimi ni mnyonge, mwenye dhambi. Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha. Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo. Bwana Yesu niwezeshe. Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu. Amen”. Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni. Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu. MUNGU AKUBARIKI !


Masomo ya matukio ya mwisho wa Dunia. Unaweza kuingia kwenye link ya kila somo.
1. KUNYAKULIWA KWA KANISA
http://davidcarol719.wordpress.com/2013/01/02/kunyakuliwa-kwa-kanisa/
2. DHIKI KUBWA
http://davidcarol719.wordpress.com/dhiki-kubwa/
3. TAJI KWA WATAKATIFU NA HARUSI YA MWANAKONDOO
http://davidcarol719.wordpress.com/2013/02/10/taji-kwa-watakatifu-na-harusi- ya-mwanakondoo/
4. KUJA KWA YESU KRISTO MARA YA PILI DUNIANI NA VITA VYA HAR-MAGEDONI
http://davidcarol719.wordpress.com/2013/02/10/kuja-kwa-yesu-kristo-mara-ya-pili-duniani-na-vita-ya-har-magedoni/
5. MIAKA 1,000 YA UTAWALA WA YESU KRISTO DUNIANI NA VITA VYA GOGU NA MAGOGU
http://davidcarol719.wordpress.com/miaka-1000-ya-utawala-wa-yesu-kristo-duniani-na-vita-vya-gogu-na-magogu/
6. UFUFU WA WAFU
http://davidcarol719.wordpress.com/187-2/
7. JEHANUM YA MOTO
http://davidcarol719.wordpress.com/jehanum-ya-moto/
8. KITI CHA ENZI KIKUBWA CHEUPE CHA HUKUMU

http://davidcarol719.wordpress.com/?s=KITI+CHA+ENZI+KIKUBWA+CHEUPE+CHA+HUKUMU

9. MBINGU MPYA NA NCHI MPYA
http://davidcarol719.wordpress.com/mbingu-mpya-na-nchi-mpya/
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . .

Zipo Baraka nyingi kwa yeyote atakaye “share “ ujumbe huu katika Facebook , Twitter n.k kwa ndugu, jamaaa na marifiki ili nao wapate nafasi ya kusoma ujumbe huu na kubarikiwa kama wewe ulivyo barikiwa. Kwasababu hii share ujumbe huu kwa kubonyeza neno“ share” lililopo chini ya “note” hii, kwa kufanya hivyo ujumbe huu utafika kwa watu wengi. Hakika, Baraka za Mungu zitakuwa nawe.

UBARIKIWE NA BWANA YESU!!!

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni