Alhamisi, 25 Septemba 2014

KUHUSU LAANA (MAKALA)

MWIMBAJI WA NYIMBO ZA INJILI JACKLINI AKIMTUKUZA MUNGU KATIKA MKUTANO WA INJILI WA GFAP ULIOFANYIKO HUKO ROMBO MKOANI KILIMANJARO JUMA LILOPITA.

KUHUSU LAANA (Kupakua/Download bonyeza link ifuatayo:
Katika waraka huu tunataka kuangalia juu ya wazo hili la “laana” itokanayo na mambo yaliyopita. Tunataka kuangalia, iwapo laana ya mtu binafsi au itokanayo na vizazi vilivyopita, inaweza kuwafungia wakristo ndani ya vifungo na kuwazuia kutokana na kupokea baraka za Mungu na Urithi wao katika Kristo. Kuanzia hapa mwanzoni mwa makala hii, hebu tuweke wazi kabisa kuwa hapa tunaongelea kuhusu mtu ambaye amehukumiwa kwa tendo la dhambi zake, akatubu na kugeuka kutoka katika dhambi zake, na akamwamini Bwana na Mwokozi Yesu Kristo kwa ajili ya wokovu wake, amezaliwa mara ya pili na kujazwa Roho wa Mungu, ameingizwa katika Agano Jipya ndani na kupitia Yesu Kristo. Hapa, kwa mtu huyo, hakuna zaidi! Hakuna kitu kilicho pungua na kwa wakristo kama ilivyoelezwa katika Agano Jipya, kuwa wakristo wa aina hiyo kama mitume walivyokuwa wakiwaandikia.

Ushahidi wa Agano Jipya

Ni kitu gani basi ambacho mitume wamewaandikia wakristo katika Agano Jipya? Wanayashughulikiaje mambo yanayojitokeza katika makanisa na watu wa Mungu? Wanayatambuaje matatizo hayo na wanatoa ushauri gani na maelekezo yapi kwao? Kwa mafundisho yoyote yale mapya, ambayo yanatoa ushauri na maelekezo yanayohusiana na wakristo, ni lazima mafundisho haya yasimamie katika misingi au yapate kuungwa mkono na maandiko ya mitume au kutoka katika mafundisho ya Yesu mwenyewe.

Kwa hiyo basi, mitume wanasemaje juu ya mafundisho yahusuyo wazo hili la “laana” zilizopita, kwamba zinaweza kuzuia maisha ya wakristo, au ya kanisa au nchi isipate kuendelea! Kwa kweli mitume hawasemi chochote kile, hakuna chochote wasemacho. Hakuna; na halikadhalika, hakuna hata mstari mmoja wa Neno la Mungu unaosema chochote kile! Wala mitume hawajaribu angalao kutamka au kugusia juu ya jambo hilo. Akili zao haziwapi kufikiria kabisa juu ya jambo hili. Yako wapi basi mausia yao wanayoyatoa kwa wakristo katika kuchunguza maisha yao ili kuhakikisha na kuwa makini sana, kwamba laana haitendi kazi yake wakati wanapokuwa katika shida ndani ya mienendo yao binafsi na kiroho? Mausio ya aina hiyo hayapo kabisa. Ni kweli kwamba Mtume Paulo anazungumza kuhusu laana, lakini anaizungumzia katika mtindo wa tofauti kabisa – yaani, anazungumzia kuhusu Kristo “akitukomboa kutoka katika LAANA ya sheria”. Tunakuja kuangalia kwa makini kuhusu jambo hili baadaye kidogo, lakini, hakuna sehemu yoyote ile ndani ya Agano Jipya lote, ambayo hata kutajwa tu kwamba laana kutoka katika mambo yaliyopita au kwamba inaweza kuzuia mwenendo wa kiroho wa mkristo au kanisa au Taifa.

Lakini sasa, sisi tutoe sababu gani tunapoona jambo hili liko kimya katika Biblia? Mafundisho hayo ya kisasa au mapya yako wazi sana na yametiririka kwa undani sana na kwa kuwa ni hivyo, basi bila shaka yangepasa kuwakilisha sehemu muhimu sana na ya lazima katika ukombozi wetu katika huyo Kristo Yesu; ikiwa jambo hili kama lingekuwa lina ukweli wowote ule.

Vitabu vingi sana vimewahi kuandika kuhusiana na jambo hili la laana, basi bila shaka, kwa hakika tungetegemea kupata misingi fulani ya mitume na ya kibiblia ndani ya mafundisho yao hayo mapya. Lakini basi, kwa nini hakuna hata mtume mmoja ndani ya Biblia anayejaribu kulitaja jambo hili katika nyaraka zake wanapoyaandikia makanisa? Je, wao walikuwa ni wajinga kiasi kwamba wameshindwa kuelewa umuhimu wa ukweli huu? Ikiwa ni hivyo basi, wao wanahusika katika kuwaacha ndani ya ujinga huo, sio tu wakristo wa vizazi vingi vijavyo, na kwa hiyo kuwazuilia uhuru wao katika Kristo. Kama ni hiyo, basi mitume wamewaachia umati mkubwa wa watu katika vifungo na giza kupitia katika karne nyingi kwa sababu ya kushindwa kwao kupokea na kufundisha mapokeo haya? Bila shaka yoyote ile, kulikuwepo na uzinzi na mila mbaya nyingi nyakati za Agano Jipya. Kwa hiyo, kwa nini basi, hawa mitume hawakuwaonya watu wa Mungu, ili wafahamu kwamba tatizo lolote lile mnalopata linatokana na laana iliyowatangulia? Kwa nini basi hawakusihi ili kuchunguza maisha yao ili waone iwapo wao wenyewe au mababu zao kama watakuwa wamehusika katika matendo ya kiShetani ambapo wengi wao wangeweza kuwa hivyo, na hivyo wangefanya hima kutubu na kuungama mambo hayo na kisha kutangaza uhuru wao katika Kirsto? Ni wapi ambapo wanashauri kufananishwa na mtu binafsi, kanisa au nchi? Ikiwa mambo hayo ni ya ukweli, basi, hilo sasa ni tatizo kubwa sana.

Hatuwezi kuachwa katika ujinga wetu, wala hatuwezi kuachwa katika vifungo! Lakini cha ajabu ni kwamba, jambo hili la laana ya mababu halitajwi mahala popote pale wachilia mbali kufundishwa pia. Elimu hiyo wanayoitoa kwa watu sio sehemu ya mafundisho ya mitume, ya Yesu Kristo wala Biblia kwa makanisa halikadhalika Agano Jipya halijafundisha hiyo kwa makanisa pia. Hakuna sehemu yoyote ile ya Agano Jipya ambapo Yesu Kristo au hata mitume wanapojaribu kutia laana ya Agano la Kale lililofanywa kati ya Mungu na Waisraeli kuitii kwa wale walioingizwa katika ufalme wa Mungu kwa kupitia uzao mpya wanavyofanya nyakati hizi.

Haya, au pengine labda wakristo wa nyakati za Agano Jipya, wao walikuwa na “usafisho zaidi na kabisa” wakati wlipookoka kuliko wakristo wa nyakati hizi za leo, na kwa hiyo hao hawakuwa na matatizo na hawakuhitaji aina hii ya mafundisho? Lakini kwa hakika mawazo hayo sio ya kweli kulingana na Neno la Mungu linavyotuonyesha. Watu walipata kuokolewa au kupokea ujumbe wa Injili kama mtu binafsi au maelfu ya watu kwa wakati mmoja. Na yawezekana pia kuwa hali ya mioyo ya wengine wao haikuwa safi au walianza vema, lakini hawakuendelea kutembea katika utiifu wa Imani na Upendo. Kama ilivyokuwa nyakati hizo halikadhalika nyakati hizi. Kimsingi, watu ni wa aina ile ile katika kila kizazi na huyapokea mambo kwa njia ya tofauti katika wokovu ambao Mungu amewapa. Na kama vile ilivyo nyakati hizi za leo, kama tusomavyo katika Agano Jipya ndivyo ilivyo kuwa pia nyakati za Agano Jipya – yaani, watu makanisani walikuwa na aina zote za matatizo yanayotofautiana: dhambi, tabia za kimwili, matendo ya uongo, uchungu, mivutano n.k. Jaribu tu kujisomea mwenyewe Wakorintho au Wagalatia, kwa mfano – utagundua haya!

Haya, iwapo wokovu wa Mungu ni ule ule leo kama vile ulivyo kuwa nyakati hizo, na iwapo mwitikio wa watu na matatizo yao ni ule ule leo, kama vile ilivyo kuwa nyakati zile za Agano Jipya; basi sasa ni kwa nini! Oho, jamani! Ni kwa nini basi Yesu Kristo mwenyewe pamoja na mitume wake hawakuwafundisha watakatifu au hata makanisa juu ya mambo hayo (au hata wale wasioamini) kwamba laana zilizopita zinaweza kuwaathiri watu wa Mungu na kuwaweka katika vifungo au giza – kama tunavyoelezwa leo na hao walimu wa kisasa? Kwa nini hawakuweza kabisa kuonyesha kwamba matatizo yetu tunayoyapata sasa tukiwa kama ni watu wa Mungu, yanatokana na laana kutoka mambo yaliyopita? Jambo hili halipaswi liwe kama vile jambo la kudhanidhani au kubuni, au kama kazi ya ubunifu ya mwanadamu. Ni jambo la hatari sana katika utata wake, kwamba ni lazima tuwe makini sana hapo katika kuyagundua mafundisho kutoka katika Agano Jipya; kwa sababu humo katika Biblia mumejazwa taarifa zote zihusuzo ukombozi wetu na wokovu katika Kristo. Lakini hata hivyo hakuna popote pale ndani yake unapoweza kuyaona mafundisho yao hayo!

Kutokana na hilo, basi hii pekee ingetosha kabisa kutuonya sisi leo, kuwa kuna kitu ambacho si cha kweli ndani ya mafundisho yao hayo na kwamba hatupaswi kuyapokea ndani ya mioyo yetu. Hii ni nyongeza yao kwenye Injili. Hii ni sumu ndani ya mioyo yetu iliyokwisha kombolewa na Kristo. Hata kama itatokea baadhi ya watu kuamini kuwa wanaweza kuipata mistari katika Agano la Kale inayounga mkono mawazo yao, bado ni lazima tutambue kuwa, kitu chochote kile kinachotakiwa kwa ajili ya wokovu na ukombozi wetu na maisha ya Ki-Mungu, kimeunganishwa na kufunuliwa hivyo pia ndani ya Agano Jipya. Kazi ya Agano la Kale ni kuonya mbele juu ya wokovu na ukombozi kwa njia mbalimbali na hii inasaidia zaidi na kufafanua na kukielezea vizuri kile kinachofundishwa ndani ya Agano Jipya. Lakini kama tunafundisha kama kwa kulazimisha kwa wokovu wetu au ukombozi kama wakristo na tunajaribu tu kupata maelezo mengine kutoka Agano la Kale kwa ajili ya kukidhi dhamira yetu ya kutaka kuungwa mkono katika jambo hilo, pasipo hata kuliona kwanza jambo hilo likifundishwa pia au kutajwa ndani ya Agano Jipya; basi ikiwa ni hivyo, hapo mafundisho yetu yatakuwa yanapingana na ukweli wa Injili.

Na hiyo sio sawa hata kidogo: hiyo ni hila, nasi tutakuwa tukiwadanganya wengine katika kufundisha hilo. Elimu yao hiyo, inapinga kabisa mafundisho ya Yesu Kirsto na ya kwamba yeye Yesu ndiye aliyesulibiwa. Hiyo ni nyongeza ya kibinadamu katika waraka wa Wagalatia. Bila shaka hakuna kupishana kabisa kati ya Agano la Kale na Agano Jipya, lakini yapo maendeleo na mabadiliko ya kimsingi. Yamechukua sehemu yake kwa sababu ya yale yaliyofanywa pale Kalvari. Kama vile ilivyo kwa makosa mengine mengi, hasa yale ya nyakati hizi za leo; mafundisho hayo hayakutokana na Biblia, bali watu wameyaanzisha au kuyabuni kutokana na mawazo yao au mtindo wao wa kufikiri, kisha wakayafasiri maandiko kulingana na matakwa ya muundo wao. Na wanapindisha na kubadilisha maana halisi ya maandiko, wakayatumia mpaka yakubaliane na muundo wa mawazo yao. Hivyo ndivyo wanavyofanya katika wanachoweza kukitumia katika Agano Jipya ili kuunga mkono mafundisho (mapokeo) yao.
Lakini hebu tutazame jinsi ambavyo watu hao wangejaribu kutafsiri baadhi ya maandiko kutoka katika Agano Jipya, ambayo ndiyo mistari wanayoitumia kunukuu. Yak.3: 7-10 na Ufu. 22:3. Hayo ni baadhi ya maandiko yanayotumiwa kunukuliwa ili kuonyesha watu kuwa laana na kulaaniwa ni vitu vinavyoendelea kuwepo leo. Kwa kadri ilivyo siyo mbaya, lakini pia wao wanaendelea kusema kuwa, kwa sababu laana inaendelea kuwepo, kwa hiyo wakristo wenyewe wanahitajika kutambua kuwa inewezekana kabisa wameshawishiwa na kuzuiwa katika maisha yao kwa laana. Lakini maandiko haya “rukii” kwenye ufahamu wa hatua hiyo wanayodai wao. Kwa kweli maandiko hayo mawili hapo juu wala hayafundishi hivyo; badala yake ingalipo inaendelea siku za leo, na watu wanafanya mambo ambayo hawapaswi kuyafanya, kwa mfano, kuwalaani wengine, na kwamba katika mbingu mpya na nchi mpya hakutakuwepo tena na laana, au tungeweza kusema kuwa, hakutakuwepo tena na hukumu – kwa ajili ya dhambi na uasi. Hata hivyo mistari hiyo hapo juu haileti uhusiano wowote kati ya matatizo ya maisha ya wakristo na laana ambayo ingeweza kuwekwa kwao au kwa mababu zao, kana kwamba hayo ndiyo iwe ni sababu ya mataizo katika maisha yao! Hakuna mahali popote pale katika nyaraka zote za Agano Jipya, ambapo hata kwa umbali tu inahesabiwa au hata kutajwa tu kwamba ndiyo sababu inayosababisha matatizo au mateso katika maisha ya wakristo, (au katika maisha ya mji au taifa). Yakobo hasemi hapo kuwa, “Tazameni, watu wanalaani, kwa hiyo mnajua laana bado inaendelea kuwepo, na kwa hiyo maisha yenu yatazuiwa kwa laana. Na kama mnalo tatizo linaloendelea katika maisha yenu, basi hilo linaweza kuwa limesababishwa na laana zilizopita. Kwa hiyo mnapaswa kuchunguza miienendo ya mababu zenu kwa makini sana ili kugundua kuwa uwezekano wa mizizi ya aina hii ya laana katika maisha yenu, na hivyo kuomba ukombozi kutokana na hilo.” Huu ni upumbavu mkubwa sana kutafsiri maandiko hayo ya Yakobo kwa jinsi hiyo. Anachokifanya Yakobo hapo katika mistari hiyo, ni kutufundisha tu kwa uwazi kwamba maneno yetu tunaposema yasiwe matamu na machungu, uchafu na usafi, baraka na laana. Jambo hilo liko wazi tu hapo, hayo ni mafundisho yenye afya nzuri tu hapo; ni mausia na kukemea kuhusiana na kuokolewa kwetu! Lakini kama nilivyotaja hapo juu, waalimu hao wanajaribu kutumia sura yoyote ile ya maandiko wanayoweza kuitumia, kisha kuipindisha na kuibadilisha, kisha kupanua maana yake halisi.

Yawezakana pia mahala pengine baadhi ya waandishi hawa wanaweza kumnukuu hata Yesu, pale anaposema, “…Wabarikini wale wanaowalaani ninyi” (Luka 6:28). Lakini katika mambo ambayo nimepata kusoma, sijaigundua hata sehemu moja ambapo waandishi hawa wanapelekea kutaja mistari hiyo pale wanapojaribu kuunga mkono mawazo yao kuhusiana na laana. Na yawezekana kuona kuwa ndiyo maana haishangazi, mafundisho hayo ya Yesu “hayapindi” kwa urahisi ili yafananishwe na mtindo wa mawazo yao. Yakobo anatueleza kuwa, anaona watu wanaendelea kulaani, wakati hawapaswi kufanya hivyo. Mafundisho hayo mapya yanasema kuwa eti ikiwa mtu bado anaendelea kulaani, kama vile Yakobo alivyosema, basi maisha ya wakristo yatadhurika kwa laana hiyo ya watu wengine. Lakini Yesu mwenyewe hasemi kuwa kama mtu atakulaani, basi “uwe mwangalifu sana, yawezekana laana hiyo ikakupata. Unauhakika kuwa hujafanya dhambi? Maana unaweza ukawa tayari uko chini ya nguvu za laana katika maisha yako, na lazima uhakikishe kwamba unataka kutoka katika laana hiyo.” Hapana. Haiwi hivyo hata kidogo; kwa sababu hata kabla ya pale Kalvari, Yesu Kristo aliwaambia watu maana halisi ya kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu na tabia yake. Yesu alisema, Ikiwa yeyote yule atawalaani, ninyi mbarikini! – Amen! Kwisha! Hakuna zaidi ya hapo. Uwabariki tu! Hayo ndiyo mafundisho yake Yesu Kristo.

Yesu hawezi kutujaza akili zetu na mawazo ya kiushirikina na udanganyifu kuhusu mambo ya uovu yanayoweza kutujia ikiwa watu watatulaani. Hakuna lolote linaloweza kutudhuru iwapo tunafuata yaliyo mema (1 Petro 3:13). Hayo ni marejeo yaliyo adimu kuhusu laana katika Agano Jipya ambamo Yesu Kristo mwenyewe aliyatoa. Kwa hakika Biblia inacho kitu cha tofauti na cha muhimu inachoweza kutufundisha. Ni kumbukumbu za pekee ndani ya Agano Jipya ambazo hutuelekeza cha kufanya na kuelezea pia kwamba tabia zetu zinapaswa kuwaje pale mtu atakapotulaani! Sasa kwa nini basi walimu hawa wanayapinga na kuyakataa yale ambayo Yesu mwenyewe anayasema kuhusu njia ya kuifuata pale mtu atakapolaaniwa? Kwa nini basi wao hawayafundishi yale ambayo Yesu Kristo anayafundisha?

Hivyo ndivyo ilivyo katika Yakobo 3:7–10, na Ufunuo 22:3. Huo ndio “Ushuhuda” wao wanaoutumia kutoka katika Agano Jipya ili kuonyesha kwamba wakristo leo wanaweza kuwa na wamo katika vifungo, giza au magonjwa – eti hiyo yote ni kwa sababu ya laana zilizopita! Na jinsi gani tunapaswa kufuatilia au kugundua laana hizo zilizopita, ambapo inaweza kwa kufanya hivyo kutupeleka nyuma zaidi ya miaka mia moja iliyopita?
Mpendwa msomaji, unafikiriaje? Je, na wewe unaamini kuwa mistari hii inatufundisha mambo hayo wayasemayo? Je, hayo ndiyo mafundisho ya Yesu au Mitume? Je, unaweza kuyapata mafundisho hayo mahala popote pale katika Agano Jipya? Ni jambo la kufurahisha kuona kuwa, bila shaka kitabu maarufu sana na chenye kuvutia na kinavyoshabikia kasoro hizi hapa ulimwenguni pote, hakijaribu hata kidogo kutoa ushahidi wowote ule katika Agano Jipya ili kuunga mkono mafundisho hayo.

TAARIFA YA UBADILISHAJI WA JINA LA BLOGU HII,KUTOKA MWAKASEGE INJILI NAKUWA HUDUMA YA UKOMBOZI GOSPLE NA ANUANI YAKE KUTOKA www.mwakasegeinjili.blogspot.com na kuwa www.ukombozig.blogspot.com

Mkurugenzi wa kampuni ya HAKI LEO ambayo ndiyo inamiliki blogu hii Oscar Samba anayo furaha kuwatangazia kwamaba siku chache zijaro jina na anuani ya blogu hii vitabadilika kama ilivyo ainishwa hapo juu.

Sababu kuu ya mabadiliko hayo  inatokana na uanzishwaji wa huduma mpya itakayokuwa chini yake naitaitwa UKOMBOZI GOSPLE.

Maono yake na malengo yake yatakuwa hatharani rasimi baada ya uzinduzi wa huduma hiyo utakao fanyika siku hiyo ya ubadilishaji wa jina hili.

Pia anaomba radhi kwa usumbufu utakao jitokeza,na tafadhali upatapo tangazo hili mtaarifu na mwenzako.